Man United yakaribia kumnasa Llorente bure

Muktasari:

Ripoti zinadai Manchester United imekubali kumpa mkataba wa miaka miwili Llorente ambaye alikuwa akilipwa Pauni 100,000 kwa wiki alipokuwa Tottenham.

MANCHESTER United imekaribia kumnasa mshambuliaji wa zamani wa Tottenham na Timu ya Taifa ya Hispania, Fernando Llorente, 34 ambaye kwa sasa ni mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba wake na Spurs Juni mwaka huu.

Llorente anaweza kusaini United muda wote kuanzia sasa kutokana na kanuni kutombana kwa vile ni mchezaji huru na ocha wa United, Ole Gunnar Solskjaer anataka kutumia uzoefu wake kuziba pengo la Romelu Lukaku aliyeuzwa kwenda Inter Milan.

Staa huyo wa zamani wa Juventus alikuwa akitakiwa na klabu za Italia lakini akasubiri kuona kama kuna ofa yoyote kutoka kwa Manchester United na sasa uhamisho wake unaweza kufanyika ndani ya siku chache zijazo.

Ripoti zinadai Manchester United imekubali kumpa mkataba wa miaka miwili Llorente ambaye alikuwa akilipwa Pauni 100,000 kwa wiki alipokuwa Tottenham.

Klabu za Ligi Kuu ya Italia, Seria A za Lazio, Inter Milan, Napoli na Fiorentina zilikuwa zikimtolea macho mashambuliaji huyo lakini mwenyewe anaitupia jicho United.