Lyanga afuzu vipimo, apewa miwili Azam

Muktasari:

Ayoub Lyanga amekuwa mmoja kati ya nyota muhimu katika kikosi cha Coastal Union na sasa anaelekea kuanza maisha mapya ndani ya Azam FC.

KLABU ya Azam imeendelea kukisuka kikosi chao na sasa wamehamia kwa mshambuliaji wa Coastal Union, Ayoub Lyanga aliyefuzu vipimo vya afya tayari kwa kusaini mkataba wa miaka miwili.

Lyanga ambaye msimu uliomalizika amekuwa katika kiwango kizuri akiipa makali ya kung'aa Coastal Union amefuzu vipimo vya afya leo asubuhi tayari kwa kusaini mkataba wa miaka miwili.

Akiwa na Coastal Union msimu uliomalizika mshambuliaji huyo amefanikiwa kufunga mabao manane na kutoa pasi za mabao nane hatua ambayo iliwavutia Azam FC.

Mshambuliaji huyo anakuwa staa wa pili wa Coastal Union kuondoka katika kikosi hicho ikiwa ni siku chache tangu kufunguliwa kwa dirisha la usajili lililokuwa wazi kuanzia jana Agosti mosi.

Jana jioni beki Bakari Nondo alianza kazi ya kukiacha kikosi cha Coastal Union baada ya kusaini mkataba wa miaka miwili kuitumikia Yanga iliyomuwinda kwa muda mrefu.

Lyanga anakuwa nyota wa tatu kujiunga na Azam katika dirisha hili akitanguliwa na viungo wawili mzawa Awesu Awesu kutoka  Kagera Sugar na  Mnyarwanda Ally Niyonzima ambao nao wote wamesaini mikataba ya miaka miwili kila mmoja.