Lwandamini aja na nyota 19 kuivaa Yanga

Muktasari:

Kwa ujumla Lwandamina aliyewahi kuifundisha Yanga, ameteua kikosi cha wachezaji wale wale ambao alisafiri nao kwenye mchezo wa marudiano katika hatua ya awali nchini Eswatini ambako waliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Green Mamba.

Dar es Salaam.  Kocha wa Zesco United, George Lwandamina anatarajiwa kutua nchini leo na kikosi cha wachezaji19, tayari kwa mchezo wa raundi ya kwanza wa kunia nafasi ya kuingia makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Yanga, Jumamosi.

Kikosi hicho kitaanza safari yake leo ambapo muda haukuwekwa wazi kwenye uwanja wa kimataifa wa Simon Mwansa Kapwepwe ambao upo Ndola huku wakitarajiwa kuingia jijini Dar es Salaam kuanzia saa 10;00 jioni.

Matumaini ya Lwandamina  yapo kwa nahodha wake, Jacob Banda ambaye ni kipa na Mburundi, Dieudonne Nthibezwa huku katika ulinzi yakiwa kwa  nyota wa kimataifa wa Kenya,  David Owino Odhiambo, Marcel Kalonda, Clement Mwape, Simon Silwimba, Mwila Phiri.

Lwandamina anafaida kwenye kikosi chake ya kurejea kwa Fackson Kampumbu ambaye alikosa michezo mingi  ya msimu uliopita kutokana na kusumbuliwa kwake na majeruhi.

Katika eneo la kiungo atatua na  mchezaji wa zamani wa Yanga, Thabani Kamusoko ambaye atakuwa anarejea  Tanzania ambako anaweza kucheza kwenye kikosi cha Zesco akiwa na John Chingandu, Enock Sabumukama  na hata Kondwani Mtonga.

Viungo wengine ni Mjapani Kosuke Nakamachi, Mkenya  Anthony Akumu pamoja na mkongwe, Mwape Mwelwa.

Mshambuliaji Mganda Umaru Kasumba ambaye bao lake liliibeba Zesco United ugenini nchini  Eswatini. Mfungaji bora wa muda wote wa timu hiyo ya Lwandamina, Jesse Were pamoja na Mnigeria, Quadri Kola ni washambuliaji watakaotua leo nchini.

Katika mchezo huo mbali na Kamusoko ambaye atacheza na timu yake ya zamani pia Winston Kalengo naye atakabiliana na Zesco United ambayo alikuwa akiichezea nyuma.