Lipuli kupiga panga wachezaji saba

Muktasari:

Lipuli licha ya kuwa miongoni mwa timu changa kwenye Ligi, lakini ilikuwa na rekodi nzuri ambapo msimu huu haikuwa kwenye hatari ya kushuka daraja kama ilivyokuwa kwa timu kongwe.

Dar es Salaam. Uongozi wa Lipuli umesema kipindi hiki cha usajili wa dirisha kubwa itapunguza wachezaji saba.

Mbali na kupunguza nyota saba, uongozi huo umebainisha kuongeza wachezaji wapya saba ili kuboresha kikosi chao kwa ajili ya msimu ujao.

Mwenyekiti wa Lipuli, Benedict Kihwelu alisema wamelazimika kupunguza wachezaji hao kutokana na kutoonyesha kiwango bora msimu uliopita.

"Uongozi utakutana katika kikao kitakachofanyika leo mchana (Juni 13), ambapo moja ya ajenda ni usajili wa timu yetu kwa msimu huu," alisema.

Alisema katika kikao hicho watajadili wachezaji wapya watakaosajiliwa kwani tayari saba wanaopewa mkono wa kwaheri wameshajadiliwa.

"Tunahitaji kuboresha kikosi chetu kionyeshe ushindani zaidi msimu ujao, msimu huu vijana walipambana, lakini kama nilivyokwishasema wachezaji saba lazima waachwe," alisisitiza.