Kumekucha usaili wa wagombea wa Yanga

Muktasari:

Uchaguzi wa Yanga unatarajia kufanyika Januari 13 mwakani, leo baadhi ya wagombea wamefanyiwa usaili na Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Soka nchini (TFF).

Dar es Salaam. Usaili wa wagombea wa Yanga umeanza leo Alhamisi kwenye ukumbi wa Shirikisho la soka Tanzania hadi sasa wagombea nafasi ya Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wamehojiwa.

Wagombea wa nafasi ya Mwenyekiti waliohojiwa ni Mbaraka Igangula na Erick Ambakisye wakati Dk Jonas Tiboroha hajafika.

Nafasi ya Makamu Mwenyekiti waliosailiwa ni Yono Kevela na Titus Osoro huku Salum Chota na Pindu Luhoyo hawajasailiwa kwani hawajafika.

Usaili huo unaendelea kwa nafasi ya wajumbe ambapo mpaka muda huu wajumbe watano wamehojiwa ambao ni Athanas Kazige, Ramadhan Said, Salim Rupia na Dominic Francis.

Wajumbe wanne ambao wamefika leo wanaendelea kusubiri kusailiwa ingawa nafasi hiyo wajumbe 17 walipita kwenye mchujo wa awali.

Kamati ya uchaguzi ya TFF itaendelea na usaili kwa wagombea wengine kesho Ijumaa.