Kocha Sharks bado haamini kuichapa Everton

Muktasari:

Sharks walikutana na Everton kwenye mechi ya kirafiki ambayo ni zawadi kwa timu inayoibuka mshindi wa kombe la Sportpesa Cup, dimba ambalo hukutanisha timu zinazodhaminiwa na Sportpesa na zile zilioalikwa.

KOCHA wa Kariobangi Sharks, William Muluya bado haamini kikosi chake kilifanikiwa kuwalima Everton wanaoshiriki Ligi Kuu ya EPL wiki moja iliyopita.

Katika kuhakikisha kweli ushindi huo dhidi ya kina Theo Walcott haukuwa wa kubahatisha, Kocha Muluya anawataka vijana wake kumpa ubingwa wa ligi msimu mpya utakapoanza.

“Historia tuliyoweka katu haiwezi kusahaulika na hakika nawapongeza vijana wangu kwa namna walivyojituma. Ushindi huo ni dhihirisho tosha kwamba tuna uwezo wa kufanikisha kile kinachoonekana hakiwezekani. Kama tumekuwa timu ya kwanza kutoka Ukanda huu kuwalima Everton, iweje tushindwe kujiwekea historia nyingine ya kutwaa ubingwa wa ligi kuu msimu mpya utakapoanza,” Muluya kahoji.

Msimu uliopita Sharks walimaliza ligi katika nafasi ya tisa huku kocha huyo akidai matokeo hayo yalichangiwa na kikosi chake kukosa wachezaji wazoefu kwani imejaa chipukizi anaojitahidi kuunda nao kikosi dhabiti.

Sharks walikutana na Everton kwenye mechi ya kirafiki ambayo ni zawadi kwa timu inayoibuka mshindi wa kombe la Sportpesa Cup, dimba ambalo hukutanisha timu zinazodhaminiwa na Sportpesa na zile zilioalikwa.

Msimu huu Sharks ndio waliibuka mabingwa wakiwashinda Everton kwa mikwaju ya penalti baada kutoka sare ya 1-1 kwenye muda wa kawaida.

Katika makala mawili yaliyopita toka dimba hilo lilipoanzishwa, Gor ndio walioibuka mabingwa wakichuana na Everton Dar es Salaam Julai 2017 na kulimwa mabao 2-1 kisha safari ya pili Novemba 2018 wakakutana nao Uingereza na kuchapwa mabao 4-0.