Kiungo ampa mchongo Kaze

KOCHA wa Yanga, Cedrick Kaze alitua jana usiku na staa wa zamani wa timu hiyo, Deo Lucas amefurahishwa na kumwambia anatakiwa kuanza kazi kwa kuboresha zaidi safu ya ushambuliaji ili iwe na makali zaidi.

Yanga mpaka sasa wako nafasi ya tatu katika msimamo wa Ligi Kuu wakiwa na pointi 13 ambapo tayari wameshacheza mechi tano na kufunga mabao saba.

Akizungumza na Mwanaspoti, Lucas alisema kazi kubwa aliyonayo kocha huyo ni kuhakikisha timu inapata mabao ya kutosha hivyo, inatakiwa kuwakomalia washambuliaji wake ili wawe fiti zaidi.

Alisema safu ya ulinzi ipo sawa hivyo kikubwa anatakiwa kuhakikisha straika wanakuwa na makali zaidi ili kwenda sambamba na kasi ya washambuliaji wa Simba ambao wa sasa wapo moto.

Kiungo huyo alisema ligi hiyo msimu huu imekuwa ngumu hivyo, ni muhimu timu ikapambana zaidi ili kwenda sawa na kasi ya Simba ambao, ndio mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Bara kwa misimu mitatu sasa.

“Timu iko sawa kikubwa kocha anatakiwa kuongeza kasi kwa washambuliaji ili kufunga mabao mengi na kusaidia kupunguza pengo kwa wapinzani hasa Simba.

“Kwangu nimefurahi sana ujio wa Kaze maana yule Zlatko Krmpotic sikumwelewa kabisa aina ya ufundishaji wake. timu ilikuwa inajichezea tu kama tungeendelea naye mambo yangekuwa magumu kwetu,” alisema Lucas.