Kisa CHAN: Yanga yaahirisha tamasha la Siku ya Mwananchi

Muktasari:

  • Yanga ipo Morogoro kwaajili ya kujiandaa na tamasha hilo ikiwa ni sambamba na maandalizi ya msimu mpya wa ligi.

Dar es Salaam. Uongozi wa klabu ya Yanga umesogeza mbele tamasha la Siku ya Mwananchi hadi hapo watakapotangaza tena ili kupisha maandalizi ya mechi Taifa Stars ya kusaka kufuzu kwa CHAN2020.

Tanzania itacheza na Kenya kati ya Julai 26 na Julai 28 katika mchezo wa kwanza wa kusaka kufuzu kwa fainali hizo za Mataifa ya Afrika kwa Wachezaji wa Ndani.

Tamasha hilo lenye lengo la kutambulisha wachezaji pamoja kufanya shughuli za kijamii lilipangwa kufanyika Julai 28 mwaka huu sasa limesogezwa mbele hadi hapo tarehe nyingine.

Akizungumza Dar es Salaam, Kaimu Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Dismas Ten alisema sababu za kusogezwa kwa tamasha hilo ni kupisha mashindano ya CHAN.

Alisema maandalizi kuelekea tamasha hilo yataendelea kama kawaida hadi hapo tamasha hilo litakapopangiwa tarehe.

"Kikosi kitaendelea na maandalizi Morogoro kambini hadi kamati ya maandalizi ya tamasha hilo itakapotangaza tarehe," alisema Tena.