Kipa Cameroon agoma kustaafu

Muktasari:

Kameni alikuwa sehemu ya kikosi cha Cameroon kilichotwaa Ubingwa wa AFCON mwaka 2002, baada ya hapo aliliongoza taifa lake kushika nafasi ya pili katika Kombe la Mabara.

KIPA  wa Timu ya Taifa ya Cameroon, Carlos  Iddris  Kameni amesema, pamoja na kuvuliwa ubingwa wa  fainali za mataifa ya Afrika hana mpango wa kustaafu soka kwa sasa.
Kipa huyo mwenye miaka 35, amekuwa sehemu ya kikosi cha timu ya Taifa ya Cameroon katika awamu sita  tofauti za fainali za AFCON, ikiwemo hii inayoendelea kutimua vumbi nchini Misri.
“Sifikirii kustaafu soka kwa sasa. Najiona  mwenye nguvu za kuendelea kucheza, pia taifa langu bado linanihitaji, nipo tayari kupigania namba pamoja na vijana wanaochipukia,” alisema  Kameni .
Kameni, ambaye aliwahi kucheza soka la kulipwa kwenye klabu za  Espanyol na Malaga, kabla ya kwenda  Uturuki kuichezea Fernabache alisema, wamepata somo kufuatia kushindwa kwao kutetea ubingwa wa AFCON.
“Tulienda Misri kutetea ubingwa wetu, tulikuwa na imani kubwa ya kufanya hivyo, kilichotokea hatukukitegemea na tumekipokea kama somo ambalo litatusaidia mbeleni,” alisema kipa huyo.
Wakati huo huo, kocha wa zamani wa timu ya Taifa ya Misri, Hassan Shehata ameelekeza lawama zake kwa  Mapharao  na shirikisho la soka nchini humo (EFA)  kwa kuondolewa kwa timu hiyo ya taifa katika  fainali za mataifa ya Afrika.
Shehata  ambaye ndiye aliyeinoa  timu hiyo ya taifa, iliyolibakisha kombe hilo kwenye ardhi yao ya nyumbani mwaka 2006, alisema  alitarajia kufanya vibaya kwa timu hiyo.
“Nilibashiri  tangu walipocheza mchezo wa kwanza kwamba hawawezi kufika popote. Kama ningekuwa kocha  kwenye kundi la wachezaji walioitwa basi ningechukua watano tu, achana na (Mohamed) Salah na  (Mahmoud Hassan) Trezeguet  hao si tatizo vipi kuhusu wachezaji wengine,” alisema Shehata.