Kha! Kagere anataka kiatu cha dhahabu

Muktasari:

Mbali na hilo alizungumzia kitendo cha watoto na watu wazima kumfuatilia kila anachokifanya uwanjani anakichukulia kama amepewa mtihani dakika anazoaminiwa na kocha kufanya kitu cha kufurahisha nafasi zao.

  KASI ya straika wa Simba, Meddie Kagere kuzifumania nyavu za wapinzani wao nyuma ya pazia kuna jambo kalifichua, anahitaji kuandika rekodi na kuchukua kiatu cha dhahabu.

Kagere amefikisha mabao 13, alipoulizwa na Mwanaspoti anawaza nini dhidi ya wapinzani wake ambao wana mabao mengi! Alijibu

“Kwanza Simba itetee ubingwa kisha nichukue kiatu cha dhahabu.

“Najua ushindani ni mkali ila bahati nzuri napenda kufanya majukumu yangu bila kuangalia jirani yangu anamiliki nini, naamini katika ubora wa kazi zangu ndio unanifanya niishi malengo yangu,” alisema.

Mbali na hilo alizungumzia kitendo cha watoto na watu wazima kumfuatilia kila anachokifanya uwanjani anakichukulia kama amepewa mtihani dakika anazoaminiwa na kocha kufanya kitu cha kufurahisha nafasi zao.

“Najali sana, nikigundua watu wanaacha kazi zao na kutenga muda kwa ajili yangu, jambo hilo linanifanya nijitoe hadi tone la mwisho sio kufunga tu bali kuhakikisha tunashirikiana timu inapata matokeo, mashabiki wa rika zote watambue nathamini mchango wao,” alisema Kagere.

Alizungumzia uzoefu wake kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika na kugusia hatua ya robo fainali, kama watakutana na Esperenc De Tunis ama timu nyingine basi haitakuwa tishio kwao.

“Timu zote zilizotinga hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika ni ngumu ila naijua vyema Esperenc De Tunis moto wao, namna ya kuupoza kwa maana timu ambayo itapangwa nayo lazima watazitambua mbinu zao,” alisema.