KMC wanacheeka kuuona mwezi

Muktasari:

Ndikumana aliongeza kwamba ushindi huo utakuwa umefungua kupata matokeo katika michezo yao ya ugenini iliyobaki kwani walikuwa wakitafuta ushindi kwa muda mrefu.

TIMU ya KMC imetengeneza rekodi yake mpya katika Uwanja wa Sokoine, Mbeya baada ya kuifunga Tanzania Prison 0-1 na kuwa ndiyo ushindi wao wa kwanza ugenini.

Nahodha wa timu hiyo, Yusuph Ndikumana alisema hawakuwahi kupata ushindi ugenini hivyo kuelekea katika mchezo huo walikuwa wamekaa chini na kuhakikisha wanapata rekodi ya tofauti.

“Unajua sisi hatujawahi kupata ushindi ugenini, huwa tunaishia kupata sare au kufungwa kwahiyo tulifanya kikao tukasema ligi haiwezi kuisha bila ya kupata pointi ugenini, naamini kabisa kikao kile na mwalimu ndicho kilichochangia sisi kwenda kuchukua pointi tatu Mbeya,” alisema.

Ndikumana aliongeza kwamba ushindi huo utakuwa umefungua kupata matokeo katika michezo yao ya ugenini iliyobaki kwani walikuwa wakitafuta ushindi kwa muda mrefu.

“Naamini kuanzia sasa njia ni nyeupe kwetu sisi kushinda ugenini, tumeshafungua njia, kilichobakia ni kutekeleza tu majukumu yetu uwanjani ili tubaki katika nafasi kwenye nzuri Ligi Kuu,” alisema.

KMC imecheza mechi 10 za nje lakini haikuwahi kupata ushindi wowote tangu Ligi Kuu msimu huu ianze mpaka hivi sasa.

Winga wa KMC, Hassan Kabunda amesema walijiwekea malengo ya kumaliza katika nafasi tano za juu na mambo yanaenda poa.