Juventus kumuuza Dybala, kumbeba Joao Felix

Muktasari:

Jina la Felix kwa sasa lipo kwenye midomo ya kila mtu hasa baada ya kuipigia Benfica hat-trick kwenye mchezo wao wa ushindi wa 4-2 dhidi ya Eintracht Frankfurt kwenye Europa League Alhamisi iliyopita

TURIN, TALIA

MAISHA ndivyo yalivyo. Juventus wamepanga kumpiga bei staa wao Paulo Dybala ili kupata pesa za kwenda kumsajili kinda matata wa Benfica, Joao Felix.

Fowadi huyo wa Kireno, Felix anayetajwa kuwa na thamani ya Pauni 87 milioni amekuwa gumzo huko Ulaya na kusakwa na klabu nyingi vigogo ikiwamo Manchester United.

Jina la Felix kwa sasa lipo kwenye midomo ya kila mtu hasa baada ya kuipigia Benfica hat-trick kwenye mchezo wao wa ushindi wa 4-2 dhidi ya Eintracht Frankfurt kwenye Europa League Alhamisi iliyopita. Felix alikaribia kutoa machozi kwa furaha ya kupiga hat-trick yake ya kwanza kwenye soka huku akiendelea kuonyesha makali makubwa kabisa ndani ya msimu huu. Kwa msimu huu, staa huyo anayetajwa kuwa ni Cristiano Ronaldo mpya, amefunga mabao 15 na kuasisti saba katika mechi 36 alizochezea Benfica msimu huu. Felix alishawahi kusema huko nyuma ndoto zake za kucheza sambamba na Ronaldo.

“Wachezaji wote bora wa Kireno wanacheza kwenye ligi kubwa za Ulaya na mimi ningependa kufanya hivyo pia. Nina ndoto mbili kubwa, nyingine ni kucheza timu moja na Cristiano Ronaldo,” alisema Felix.