Hesabu za TFF zamchanganya Masau Bwire

Muktasari:

Adhabu hio kwa Masau Bwire imetolewa kwa kuzingatia Kanuni ya 14(49) ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Dar es Salaam.Baada ya Bodi ya Ligi kumpiga faini Sh 200,000, Masau Bwire kwa kosa la kuingia ndani ya Uwanja kushangilia ushindi wa Ruvu Shooting dhidi ya Yanga Agosti 28, mwaka huu amepiga adhabu hiyo.

Afisa habari huyo wa Ruvu Shooting alisema Bodi ya ligi wametoa uamuzi huo bila kumhoji na kujua kwanini alikua pale.

"Mimi sikwenda uwanjani kushangilia mpira, niliingia baada ya kuitwa na mwandishi wa Azam (Ngoda), ili kufanya mahojiano na ndipo wachezaji wa Ruvu wakaanza kunikumbatia sasa ulitaka nisiwakumbatie na kuwafukuza?" alisema Masau na kuongeza kuwa

"Sheria za ligi zinasema tumheshimu mdhamini wa Ligi na tufuate taratibu zao, na mimi niliwaheshimu watu wa Azam kama wadhamini ndio maana nikawepo eneo lile baada ya mechi kumalizika."

Masau Bwire ameiomba Bodi ya ligi ifanye marejeo ya Adhabu hiyo, lakini ameambiwa inabidi atoe sh1 milioni ili marejeo yafanyike jambo ambalo amepata kizungumkuti.

"Nimewaomba wafanye marejeo ya adhabu hiyo, lakini cha kushangaza ni kwamba nimeambiwa ninatakiwa kutoa shilingi milioni moja ili marejeo yafanyike sasa kwa hesabu za kawaida hapo kati ya 200,000 za faini na 1000000, ya kufanyia marejeo nini bora?," aliongeza.

Adhabu hio kwa Masau Bwire imetolewa kwa kuzingatia Kanuni ya 14(49) ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.