He! Guardiola asema kuhusu kufutwa kazi

Muktasari:

Kwenye michuano mingine, Man City imefika fainali ya Kombe la Ligi, bado ipo kwenye Kombe la FA na bila ya shaka, Guardiola mwenyewe pamoja na bodi ya timu hiyo siku zote wamekuwa wakiwaza kubeba taji la Ligi ya Mabingwa Ulaya.

MANCHESTER,ENGLAND. KOCHA wa Manchester City, Pep Guardiola amesema angeshafutwa kazi kwenye klabu hiyo kama timu yake ingekuwa tayari imeshatupwa nje ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Real Madrid.

Man City imekuwa na msimu wenye mambo mengi, ikipambana kwenye kuwania mataji yote, isipokuwa kwenye matumaini tu ya kutetea ubingwa wa Ligi Kuu England baada ya kuachwa pointi nyingi na vinara Liverpool.

Kwenye michuano mingine, Man City imefika fainali ya Kombe la Ligi, bado ipo kwenye Kombe la FA na bila ya shaka, Guardiola mwenyewe pamoja na bodi ya timu hiyo siku zote wamekuwa wakiwaza kubeba taji la Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Kwenye hilo, wanakabiliwa na mtihani mzito wa kuwakabili vinara wa La Liga, Real Madrid kwenye hatua ya 16 bora na Guardiola anataka ushindi.