Hazard akiri kuwa kibonge Madrid

Muktasari:

Hata hivyo, kumekuwa na madai kwamba bado Hazard hajarudi kwenye ule ubora ambao uliwafanya Real Madrid kutoa pesa kunasa saini yake ambapo dau hilo linaweza kupanda na kufikia Pauni 150 milioni.

MADRID, HISPANIA . SUPASTAA, Eden Hazard amekiri kwamba alikuwa ameongezeka uzito wakati anajiunga na Real Madrid.
Na kwamba Mbelgiji huyo hakuwa ameongezeka kilo chache wakati anakamilisha uhamisho wake huo wa Pauni 89 milioni kutoka Chelsea katika dirisha lililopita la majira ya kiangazi.
Hazard amefichua kwamba aliongezeka kilo tano wakati anatua Bernabeu na ndio maana picha alizopigwa kwa wakati huo alionekana kuwa kibonge, lakini alizikata na kurudi kwenye uzito wake kwa muda wa siku 10 tu. Hazard alijisahau na kufanya mwili kuongezeka baada ya kuisaidia Chelsea kuichapa Arsenal na kubeba Europa League, Mei mwaka huu.
Hata hivyo, kumekuwa na madai kwamba bado Hazard hajarudi kwenye ule ubora ambao uliwafanya Real Madrid kutoa pesa kunasa saini yake ambapo dau hilo linaweza kupanda na kufikia Pauni 150 milioni.
Lakini, mwenyewe anaamini kwamba amezidi kuwa kwenye kiwango chake kizuri kila siku chini ya kocha Zinedine Zidane.
Hazard alisema: "Kuhusu uzito wangu, sitaki kuficha ukweli. Nilipoenda likizo, nilikuwa likizo kweli.
“Mimi ni mtu ninayeongezeka uzito kwa haraka sana na kupungua kwa haraka pia. Nilikuwa Lille, kipindi hicho nina miaka 18, nilikuwa na uzito wa kilo 72. Baada ya hapo, niliongezeka na kuwa kilo 75. Kuna siku moja nilipima nikajikuta na kilo 77, lakini kwenye kipindi cha mapumziko, nilikuwa na kilo 80. Nilizipunguza kilo hizo ndani ya siku 10 tu.”