Panachimbika Ligi Daraja la Kwanza leo
Muktasari:
Kaimu Katibu Mkuu wa TFF, Wilfred Kidao amesema, haitavumilia kitendo chochote kitakachojihusisha na hujuma ya upangaji wa matokea na watawachukulia hatua kali wale wote watakaojihusisha na matukio hayo.
KIVUMBI cha Ligi Daraja la Kwanza kinaendelea leo Jumamosi ambapo nyasi za viwanja nane zitawaka moto, lakini TFF imetoa onyo kali kwa wale wataalamu wa kupanga matokeo wakijaribu, wataadhibiwa.
Kaimu Katibu Mkuu wa TFF, Wilfred Kidao amesema, haitavumilia kitendo chochote kitakachojihusisha na hujuma ya upangaji wa matokea na watawachukulia hatua kali wale wote watakaojihusisha na matukio hayo.
Waamuzi watakaochezesha mechi hizo wametakiwa wajikite katika kuchezesha kwa haki na Tff imeviandikia barua vyombo vyote vya ulinzi na usalama kufuatilia hatua hizo za michezo ya mwisho.
Katika michezo hiyo ya kundi A, Uwanja wa Filbert Bayi kutakuwa na mchezo kati ya Kiluvya United dhidi ya Mgambo JKT wakati Mvuvumwa watacheza na JKT Ruvu Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.
Mechi nyingine ni za kundi B, Coastal Union itaikaribisha Mufindi United kwenye Uwanja wa Mkwakwani, JKT Mlale itacheza na Mawenzi Market Uwanja wa Majimaji na Mbeya Kwanza itakipiga dhidi ya KMC Uwanja wa Sokoine.
Katika michezo ya kundi C, Toto Africans itacheza na JKT Oljoro, Rhino Rangers na Dodoma FC kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi na Biashara United itacheza n Alliance School.