Haaland anaingia, Benzima anatoka

Muktasari:

Haaland, ambaye amepachika mabao 12 mpaka sasa tangu ametua Borussia Dortmund kwenye dirisha dogo la Januari akitokea Red Bull Salzburg.

Madrid, Hispania . HARAKATI za usajili huko Ulaya zinakwenda kwa kasi sana huku wababe wakiweka mikakati sawa ili kuwanasa wachezaji wanaowataka.

Huko Real Madrid msimu ujao kikosi chake kinaweza kuonekana kwenye sura tofauti kwani, kuna mabadiliko makubwa yatafanyika. Kwa sasa macho yote yapo kwenye kuisuka upya safu yake ya ushambuliaji na kinda wa Borrsuia Dortmund, Erling Haaland, amekuwa kivutio.

Miamba hiyo ya La Liga imefanya usajili mkubwa kwenye misimu miwili iliyopita, lakini mastaa waliotua wameonekana kushindwa kuonyesha kila kilichotarajiwa.

Kwa sasa Kocha Zinedine Zidane amekuwa akitegemea huduma ya Karim Benzema katika kupachika mabao huku staa waliyemnasa kwa dau la Euro 62 milioni, Luka Jovic kutoka Eintracht Frankfurt akionekana kuchemka vibaya.

Lakini, Zidane ameamua kufanya maamuzi magumu na mpango uliopo kwa sasa ni kuwafungulia mlango baadhi ya mastaa wake akiwemo Benzema na kumshusha kikosini kwake Haaland.

Haaland, ambaye amepachika mabao 12 mpaka sasa tangu ametua Borussia Dortmund kwenye dirisha dogo la Januari akitokea Red Bull Salzburg.

Kinda huyu mwenye miaka 19, anaweza kuondoka Dortmund kwa dau la Euro 63 milioni tu kwa mujibu wa kipengele kilichopo kwenye mkataba wake.

Kwa maana hiyo, Haaland anaweza kupatikana mwishoni mwa msimu kwa dau dogo kabisa kulinganisha na uwezo wake uwanjani.

Hata hivyo, kinda huyo ambaye anasimamiwa na wakala tajiri Mino Raiola, anaweza kuziingiza vitani klabu kubwa Ulaya ikiwemo Barcelona, Manchester United, Liverpool na Bayern Munich.