Ferdinand atamani Maguire kupumzishwa

Manchester, England. Rio Ferdinand amemwambia kocha Ole Gunnar Solskjaer: “Mtoe kwa muda Harry Maguire katika ‘moto’.”

Mchezaji huyo wa zamani wa Manchester United, amependekeza kuwa Maguire anatakiwa kupumzishwa kwa ajili ya manufaa yake, baada ya kuonyeshwa kadi nyekundu juzi alipokuwa akiitumikia England dhidi ya Denmark.

Ferdinand, ambate sasa ana miaka 41, alisema: “Bila shaka kwa sasa ni rahisi kumuona akipitia katika changamoto za uwanjani. Hakuna anayependa kumwona katika hjali hii

“Kama unahitaji kucheza vizuri, kuwa na hali ya kujiamini uwanjani ni suala la msingi. Hilo amelikosa kwa sasa na linahatarisha ubora wake uwanjani.

“Kutokana na hali hii, ambalo hata mimi niliwahi kulipitia, kuna wakati unahisi unatakiwa kutolewa katika ‘jiko la moto’ ili upoe kidogo.”

Lakini mchambuzi huyo wa soka, Ferdinand aliongeza: “Kuna wakati hata mchezaji mwenyewe unatakiwa kujitoa katika moto hata mchezo mmoja ukikaa nje inasaidia kukurudisha mchezoni.

“Ni suala la kujipa muda wa kukaa pembeni na kupitia makosa yako, kuangalia kila kitu ulichofanya.

“Ukiwa unacheza mechi baada ya mechi na hasa unapocheza mechi katika kila baada ya siku tatu ama nne ni ngumu kuangalia ulichokifanya.”