Duh! Pepe amchomolea mbavuni Unai Emery

Muktasari:

  • Pepe kwa sasa ni mchezaji huru baada ya kuachwa na Besiktas mwezi uliopita na mwanzoni ilielezwa angerudi kwao huko Ureno kwenda kujiunga na vinara wa ligi ya nchi hiyo, FC Porto.

MONACO, UFARANSA . SI unajua Kocha Unai Emery kwa sasa anasaka beki wa kati huko kwenye kikosi chake cha Arsenal ili kuweka mambo sawa.Basi bana huko na huko, akavamia kwa beki wa zamani wa Real Madrid, Pepe akimtaka aje kwenye kikosi chake.

Alichokutana nacho anakijua mwenyewe. Emery ameambiwa wazi na Pepe hana mpango wa kwenda kujiunga na Arsenal na anachotaka kwa sasa ni kwenda AS Monaco kuwa chini ya Thierry Henry.

Pepe kwa sasa ni mchezaji huru baada ya kuachwa na Besiktas mwezi uliopita na mwanzoni ilielezwa angerudi kwao huko Ureno kwenda kujiunga na vinara wa ligi ya nchi hiyo, FC Porto.

Lakini L’Equipe linafichua Pepe kwa sasa yupo kwenye hatua za mwisho kabisa kujiunga na Monaco, ambayo ipo chini ya staa wa zamani wa Arsenal na Barcelona, Henry, ambaye ndiye kocha. Arsenal ilitaka kufanya ujanja wa kumnasa beki huyo wa kati, lakini ikakutana na neno ‘no’ kutoka kwa beki huyo mshindi wa Euro 2016. Arsenal ipo sokoni kwa sasa kusaka beki wa kati baada ya kukumbwa na majeruhi wengi.