Dodoma FC yaipiga bao Yanga

Muktasari:

Mkandala alitamba mwanzoni mwa msimu uliopita hali iliyowafanya baadhi ya viongozi wa Yanga kutaka huduma yake katika dirisha dogo.

DODOMA FC iliyopanda daraja msimu huu kucheza Ligi Kuu Bara imenasa saini ya kiungo Cleofas Mkandala kutoka Prisons aliyekuwa anahusishwa kujiunga Yanga kwa muda mrefu.

Wakati ligi ikiwa inaendelea msimu uliopita, kiungo huyo alikuwa akitajwa zaidi kutua Yanga lakini dili hilo lilionekana kuota mbawa baada ya kusajiliwa Zawadi Mauya.

Kupitia taarifa iliyotolewa na Afisa Habari wa klabu hiyo, Ramadhan Juma imesema wamesajili nyota wapya ambao ni Mkandala (Prison), Michael Chinedu (Alliance) na Seif Karie (Lipuli).

"Baada ya dirisha kubwa la usajili kufunguliwa, timu imeendesha zoezi la usajili kwa mujibu wa mapendekezo  ya benchi la ufundi,".

Licha ya kusaini wachezaji hao, Dodoma Fc imewaongezea mikataba wachezaji wao Emmanuel Mseja, Hussein Msalanga, Anderson Solomon, Hassan Kapona, Mbwana Kibacha, Rajabu Seif, Steven Mganga, Jamal Mtegeta, Deusdelius Kigawa, Santos Thomas na Khamis Mcha.

Kwa upande wa wachezaji walioachwa ni Yusuf Abdul, Joseph Mapembe, Hamad Kibopile, Rajabu Kibera, Joshua Soka, Aziz Gillah, Shabani Mocka, James Mendy, Ismail Makorosa, Moshi Mrisho, Mohamed Kirua na Ramadhan Mohamed ambaye amerejeshwa Azam Fc baada ya mkataba wake wa mkopo kumalizika.