Conte: Aku! Messi haji kwetu jamani

MILAN, ITALIA. KOCHA mkuu wa Inter Milan, Antonio Conte amezikanusha taarifa zinazodai kwamba miamba hiyo ya Serie A ipo bize kwenye mpango wa kunasa huduma ya supastaa wa Barcelona, Lionel Messi wakati dirisha lijalo la uhamisho wa majira ya kiangazi litakapofunguliwa.

Kumekuwa na ripoti siku za karibuni kwamba miamba hiyo ya Italia imekuwa na uhakika mkubwa wa kunasa huduma ya supastaa huyo wa Kiargentina wakati mkataba wake utakapofika tamati Nou Camp msimu ujao.

Hata hivyo, kocha Conte alisema uvumi huo unatia chachu tu kwenye soka, huku akisisitiza hakuna uwezekano wowote wa wababe hao wa Serie A kukamilisha dili la kumsajili fowadi huyo mwenye umri wa miaka 33.

“Tunazungumzia vitu visivyowezekana kwenye soka, hayo mambo kwa sasa hayaonekani kabisa kama yanahusiana na Inter,” alisema.

“Hakuna asiyemtaka Messi. Lakini, mambo yapo wazi, yupo mbali sana na kujiunga na Inter.”

Messi aliikosoa timu yake baada ya kuchapwa 2-1 na Osasuna kwenye La Liga, Julai 16 na kufanya miamba hiyo ya Catalan kutoa mwanya kwa mahasimu wao, Real Madrid kunyakua taji hilo msimu huu.