Chuji aaga Coastal Union asaka timu mpya

Muktasari:

Kiungo Athumani Idd 'Chuji' ameibuka na kuweka wazi mpango wake msimu ujao ni kucheza timu nyingine baada ya kucheza kwa muda mrefu Coastal Union.

Dar es Salaam. Kiungo Athuman Idd 'Chuji' ni kama ameaga Coastal Union na sasa anasaka timu nyingine kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Bara.

Chuji kiungo anayesifika kuwa na pasi za rula yaani anapopiga huwa inamfikia mlengwa na alicheza kwa mafanikio klabu za Simba na Yanga pamoja na Taifa Stars.

Alisema, anataka kubadili upepo kwenda kucheza timu nyingine baada ya mkataba wake na Coastal Union kumalizika.

"Mkataba wangu na Coastal Union umeisha sifikirii kama naweza kuongeza mkataba mpya kwa sababu nimeshacheza kwa kipindi kirefu,"alisema Chuji.

Alisema, kwa sasa anaangalia timu itakayomfata vizuri ili acheze kwa ajili ya msimu ujao wa ligi.

"Sijafanya mazungumzo na timu nyingine yoyote lakini watakaonifata na pesa yao ikiwa nzuri nitafanya kazi,"alifafanua Chuji.