Chirwa asaka rekodi

Muktasari:

Septemba 18, 2013, alifunga idadi hiyo ya mabao katika ushindi wa mabao 6-0 wa Simba dhidi ya Mgambo JKT, akafunga tena idadi hiyo Februari Mosi, 2014 wakati Simba ilipoifunga JKT Oljoro kwa mabao 4-0 na baadaye alipotua Yanga, Aprili 8, 2015 alipachika mabao matano katika ushindi wa mabao 8-0 dhidi ya Coastal Union.

Dar es Salaam/Mwanza. Mabao matatu ‘hat trick’ aliyofunga dhidi ya Alliance FC jana, yamemfanya mshambuliaji wa Azam FC kujitengenezea mazingira ya kuifikia ama kuvunja rekodi iliyowahi kuwekwa na nyota wa Burundi, Amissi Tambwe katika Ligi Kuu Bara.

Mabao hayo yamemfanya Chirwa afikishe idadi ya mechi tatu ambazo amefunga ‘hat trick’ katika mchezo mmoja ikiwa ni nusu ya kile kilichofanywa na Tambwe aliyewahi kuzitumikia Simba na Yanga kwa nyakati tofauti.

Kabla ya mchezo wa jana uliofanyika Uwanja wa Nyamagana na Azam kupata ushindi wa mabao 5-0, aliofunga idadi hiyo dhidi ya Alliance, Chirwa aliwahi kufanya hivyo katika ushindi wa mabao 5-0 ambao Yanga iliupata dhidi ya Mbeya City, Novemba 18,2017 na akaja kurudia tena Februari 6, 2018 alipoiongoza Yanga kuichapa Njombe Mji kwa mabao 4-0. Tambwe anayeongoza kwa kufunga idadi ya mabao matatu katika mchezo mmoja mara nyingi, amefanya hivyo katika michezo sita tofauti pindi alipoichezea Simba na baadaye Yanga.

Septemba 18, 2013, alifunga idadi hiyo ya mabao katika ushindi wa mabao 6-0 wa Simba dhidi ya Mgambo JKT, akafunga tena idadi hiyo Februari Mosi, 2014 wakati Simba ilipoifunga JKT Oljoro kwa mabao 4-0 na baadaye alipotua Yanga, Aprili 8, 2015 alipachika mabao matano katika ushindi wa mabao 8-0 dhidi ya Coastal Union.

Aprili 27, 2015 alifunga ‘hat trick’ wakati Yanga ilipoichapa Polisi Morogoro kwa mabao 4-0, akafunga tena wakati timu yake ilipoibuka na ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Stand United, Disemba 19, 2015 na ‘hat trick’ yake ya mwisho ilikuwa ni dhidi ya Majimaji FC mnamo Januari 21, 2016 wakati Yanga iliposhinda mabao 5-0.

Katika mchezo wa jana dhidi ya Alliance, Chirwa alifunga mabao hayo katika dakika ya 2, 24 na 67 huku mabao mengine mawili yakifungwa na Shaban Chilunda dakika ya 31 na 52.

Matokeo hayo yameifanya Azam kufikisha pointi 19 na kupanda hadi nafasi ya nne katika msimamo wa Ligi Kuu Bara huku Alliance wakishuka hadi nafasi ya sita na pointi zao 17.

Katika mchezo mwingine, kipigo cha mabao 3-1 ilichokipata nyumbani kutoka kwa Mtibwa Sugar, kimeifanya Kagera Sugar ishindwe kukwea kileleni mwa msimamo wa ligi na kuipiku Simba inayoongoza.

Mabao ya Haruna Chanongo aliyepachika mawili na Juma Nyosso aliyejifunga, yaliifanya Kagera Sugar ibakie nafasi ya pili na pointi zake 23, huku bao lao la kufutia machozi likifungwa na Awesu Awesu.

Mbao FC iliutumia vyema uwanja wake wa nyumbani wa CCM Kirumba baada ya kuichapa KMC kwa mabao 2-0, Biashara United ikishinda 1-0 kwa Lipuli na JKT Tanzania wakaipiga Ruvu Shooting 2-1. Mkoani Mbeya, wenyeji Mbeya City walikubali kipigo cha 1-0 mbele ya Mwadui.

Imeandikwa na Charles Abel, Saddam Sadick na James Mlaga.