Bigirimana alianzisha mapema

STRAIKA wa Namungo, Bigirimana Blaise amelianzisha mapema kwa kumchimba mkwara Meddie Kagere kwamba msimu huu wa Ligi Kuu Bara atakula naye sahani moja ili kumpora tuzo ya Mfungaji Bora aliyoishikilia kwa misimu miwili mfululizo.

Blaise ndiye mchezaji wa kwanza msimu huu kuifunga bao katika Ligi Kuu iliyoanza wikiendi iliyopita, pia akiwa nyota wa kigeni kutupia nyavuni, alisema mabao 10 aliyomaliza nao msimu uliopita anataka yazidi maradufu ili kubeba tuzo anayoishikilia Kagere aliyeitetea msimu uliopita kwa mabao 22. Katika msimu wa kwanza wa kucheza Ligi Kuu, Kagere alitwaa pia kwa kufunga mabao 23.

Akizungumza na Mwanaspoti, Blaise alisema msimu huu amejipanga kuhakikisha anafumania nyavu vilivyo ili kuisaidia timu yake sambamba na kuwa mfungaji bora katika msimu huu, kazi aliyoanza kwa Coastal alipofunga bao pekee lililoifanya Namungo kushika nafasi ya nne kama waliyomaliza nayo msimu uliopita.

“Kwa misimu miwili iliyopita, Kagere ndiye alikuwa mfungaji bora, ila safari hii nataka iwe zamu yangu, uwezo ninao nimejipanga, kwa kushirikiana na wachezaji wenzangu naamini nitafunga, na nitajitahidi kujituma mazoezini ili kumfanya mwalimu anipe nafasi kutimiza lengo langu,” alisema Blaise aliyefunga mabao 23 tangu aanze kucheza msimu akianza klabu za Stand United, Alliance kabla ya kunyakuliwa na Namungo msimu uliopita.