Benchi lampasua kichwa kipa JKT Tanzania aingia chimbo

Muktasari:

Kipa wa JKT Tanzania, Abobakar Barwany amecheza mechi tatu tu kati ya 29 ilizocheza timu hiyo hadi sasa katika Ligi Kuu Tanzania Bara.

Mwanza.Kipa wa JKT Tanzania, Abobakar Barwany amesema amecheza mechi tatu pekee za Ligi Kuu Tanzania bara hivyo anatakiwa kujituma zaidi kutokana na ushindani mkubwa wa namba katika kikosi chao.

Kipa huyo alisajiliwa na JKT Tanzania akitoka Geita Gold msimu uliopita akiwa moja ya makipa bora ligi daraja la Kwanza akicheza mechi 15 kati 22 bila ya kuruhusu bao langoni kwake.

Barwany alisema anatakiwa kupambana vilivyo kwani katika kikosi chao wapo makipa wanne wote wako vizuri jambo ambalo limefanya ushindani wa namba kuwa mkubwa haswa kwa upande wake.

 “Nimecheza mechi tatu tu za Ligi Kuu tangu nimesajiliwa hapa JKT Tanzania natakiwa kupambana sana kwani kama mchezaji najisikia vibaya kukaa benchi kila mchezo kikubwa hapa kuna ushindani mkubwa wa namba hivyo natakiwa kukabiliana nao,” alisema Barwany.

Alisema kwa sasa amekuwa akijifua mara tatu kwa siku ili kujiweka fiti ili ligi itakaporejea aweze kumshawishi kocha kumwamini na kumpa nafasi.