Ben Paul aibuka kivingine

Muktasari:

Ben Paul amesema kukaa kwake kimya hakumaanishi kwamba ameishiwa cha kufanya kwenye muziki wa Bongo Flava badala yake anaumiza akili namna ya kuandaa kazi nzuri itakayokuwa inapendwa na mashabiki wake.

BAADA ya kimya kingi, msanii wa kizazi kipya Ben Paul ametoa kibao kipya kinachojulikana kwa jina la Sana, ndani yake kikiwa kimebeba maudhui ya mapenzi, nyimbo hiyo ameshirikiana na Timaya kutoka Nigeria.
Ben Paul amesema kukaa kwake kimya hakumaanishi kwamba ameishiwa cha kufanya kwenye muziki wa Bongo Flava badala yake anaumiza akili namna ya kuandaa kazi nzuri itakayokuwa inapendwa na mashabiki wake.
Anasema kwa aina yake ya muziki anaoufanya hajaona wa kumuumiza akili na anaamini nyimbo zake za zamani bado zinaendelea kuishi kwa mashabiki wake.
"Nyimbo hii ni kali naamini mashabiki wataifurahia, pamoja na kwamba ni ya mapenzi lakini ndani yake ina funzo kubwa kwa mtu yoyote ambaye ataisikiliza kwani naamini hakuna binadamu asiyependa.
"Bado naendelea kufanya muziki na nitaendelea kuwepo kwenye ushindani, nitabakia kuwa Ben Paul na mwingine atabakia kuwa yeye, kinachotakiwa ni kazi nzuri ambayo itakuwa inafunza, inaelimisha jamii.
"Kuna nyimbo nyingine nzuri ambazo nitaendelea kuzitoa zitakazokuwa zina ushindani sokoni, kikubwa mashabiki wangu wakae muda wa kusikia mambo mazuri kutoka kwangu,"anasema.