Beki Ajax azivuruga Barcelona, Manchester United

Muktasari:

Nahodha huyo wa Ajax Amsterdam ametoa kauli ya utata, baada ya kudai kuwa hata kama atajiunga na Man United, lakini anaweza kucheza Barcelona baadaye.

London, England. Beki Matthjis de Ligt amezidi kuzivuruga Manchester United na Barcelona zinazowania saini yake katika usajili wa majira ya kiangazi.

Nahodha huyo wa Ajax Amsterdam ametoa kauli ya utata, baada ya kudai kuwa hata kama atajiunga na Man United, lakini anaweza kucheza Barcelona baadaye.

De Ligt alisema ni ndoto ya kila mmoja kucheza Barcelona licha ya kuwa na mabeki bora duniani.

Kauli ya kinda huyo mwenye miaka 19 aliyeibukia katika mechi za Ligi ya Mabingwa Ulaya inaweza kuongeza vita baina ya miamba hiyo ya soka ambayo kila moja inataka saini yake.

Nahodha huyo alisema ni fahari kucheza pembeni kwa kiungo Frenkie de Jong na Lionel Messi.

“Barcelona ina mabeki bora ingawa ni jambo jema kucheza na De Jong na Lionel Messi, lakini unapaswa kuangalia ushindani wa namba,” alisema De Ligt.

Kinda huyo alicheza vizuri kwa asilimia 100 katika kikosi cha Ajax msimu uliopita. Mkataba wa De Ligt unatarajiwa kumalizika mwaka 2021.