Bayern Munich wakataa kumpa kazi Arsene Wenger

Muktasari:

Kwa mujibu wa gazeti maarufu la huko Ujerumani, Bild, Wenger alimpigia simu bosi wa Bayern Munich, Karl-Heinz Rumenigge kutangaza anataka kazi ya kuinoa timu hiyo, lakini Rumenigge amegoma kukubaliana na ombi la Wenger la kuchukua mikoba ya Kovac.

MUNICH, UJERUMANI . NDIO hivyo tena. Arsene Wenger amepiga sana sala kupata kazi ya kuinoa Bayern Munich, lakini mabosi wa timu hiyo wamekutana na kutoka na jibu moja tu, hapana.

Kwa kifupi tu Bayern Munich imegoma kutoa nafasi kwa kocha huyo wa zamani wa Arsenal, kuwa bosi wao mpya katika kikosi hicho baada ya kumfuta kazi Niko Kovac.

Kwa mujibu wa gazeti maarufu la huko Ujerumani, Bild, Wenger alimpigia simu bosi wa Bayern Munich, Karl-Heinz Rumenigge kutangaza anataka kazi ya kuinoa timu hiyo, lakini Rumenigge amegoma kukubaliana na ombi la Wenger la kuchukua mikoba ya Kovac.

Wenger amekuwa hana kazi tangu alipoachana na Arsenal msimu wa 2017-18 baada ya kudumu kwenye timu hiyo kwa kipindi cha miaka 22. Wenger anataka kurudi kwenye kiti cha ukocha, lakini taarifa zinadai huko nyuma alikataa ofa kibao za kazi baada ya kuachana na maisha ya Emirates. Hansi Flick ndiye kocha wa muda kwa kwenye kikosi hicho ambapo aliongoza Bayern kushinda 2-0 dhidi ya Olympiacos kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya Jumatano iliyopita.

Shughuli pevu itamkabili leo Jumamosi wakati atakapowakabili Borussi Dortmund huko Allianz Arena. Mabosi wa Bayern wanamfikiria Kocha wa PSG, Thomas Tuchel na yule wa Ajax, Erik ten Hag huku Max Allegri na Jose Mourinho nao wakihusishwa.