Balotelli kwa visa amtumbukiza mtu baharini

Muktasari:

  •  Kulikuwa na muinuko kidogo uliojengewa kutoka usawa wa nchi kavu na baharini alikojitosa kibonge huyo. 

Dar es Salaam. Mshambuliaji wa zamani wa Manchester City, Mario Balotelli ameingia matatani na mamlaka za Italia baada ya kucheza kamari ya kumlipa pauni 1,800 mmiliki wa baa kuendesha pikipiki yake hadi baharini.

Balotelli anaponda raha nyumbani kwao Italia, anadaiwa kumpa pesa, mmiliki wa baa ya mtaani ili aendeshe pikipiki yake aina Vespa hadi ndani ya maji.

Nyota huyo amezoeleka kwa utukutu, alitoa Paundi 1,800 zilizomtia ukichaa mmiliki huyo wa baa akiwa na vazi la ufukweni aliwasha pikipiki hiyo mara moja na kutumbukia nayo baharini.

Baada ya kutekeleza alichotaka Balotelli, mmiliki huyo wa baa ambaye kimuonekano ni kibonge, alijichukulia kiasi hicho cha fedha na kuacha watu wakimshangaa.

Pikipiki hiyo iliyotumbukizwa baharini ina thamani ya Paundi 540 hivyo kupitia kiasi alichovuna alikuwa anauwezo wa kununua nyingine.

Kinachodaiwa kumweka matatani, Balotelli ni kipande cha video kilichosambaa kinachomwonyesha mmiliki wa baa huyo akijitosa na pikipiki yake baharini.