Bale atishia nyau mabeki

LONDON, ENGLAND. SUPASTAA, Gareth Bale amewatisha mabeki kwenye Ligi Kuu England kwamba bado hajaanza mambo yake baada ya kucheza mechi yake ya kwanza akiwa amerejea kwenye kikosi chake cha zamani cha Tottenham Hotspur.

Bale alicheza kwa dakika 60 akiisaidia Spurs kuichapa LASK kwenye Europa League na hata kusababisha bao wakati krosi yake ilipombabatiza mchezaji wa timu pinzani na kujifunga.

Hata hivyo, staa huyo wa kimataifa wa Wales alisema bado anahitaji muda wa kurudi kwenye ubora na hapo atakapokuwa sawa basi Spurs itarudi kwenye makali yake ya kuwa washindani wa mataji ndani ya England na Ulaya.

Bale alisema: “Hizi ni zile nyakati nitazitumia kurudi kwenye ubora wangu. Naamini nitatumia wiki chache kurudi katika kiwango changu.

“Ni wakati wa kujaribu kuzoea mambo na nitafanya mazoezi kwa nguvu zote ili kuwa bora. Nitapoanza kuwa fiti na kucheza kila dakika mchango wangu utakuwa mkubwa kwenye timu. Limekuwa jambo jema kwangu kurudi na kufurahia soka. Hii timu ina kikosi kizuri na kocha ni mzuri sana.”

Hata hivyo, kwenye mechi hiyo Bale alifunikwa na staa mwingine aliyecheza mechi yake ya kwanza, Carlos Vinicius, ambaye alitengeneza mabao mawili na hivyo kuonekana ni chaguo bora la mbadala wa staa wao wa mabao Harry Kane.