Azam kuitumia Yanga kujinoa kwa Lipuli

Muktasari:

  • Azam ilikuwa timu ya kwanza kutinga fainali ya kombe la FA kwa kuifunga KMC bao 1-0 huku wakifuata Lipuli iliyoiifunga Yanga mabao 2-0.

Dar es Salaam. Kocha wa Azam, Meja Mstaafu Abdul Mingange amesema mchezo wao uliosaliwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Yanga, utakuwa sehemu ya kujiandaa na fainali ya kombe la FA, Juni mosi.

Azam wanatarajia kucheza fainali ya kombe la FA maarufu Azam Sports Federation Cup kwenye uwanja wa Ilulu, Lindi kwa mara ya kwanza dhidi ya Lipuli.

Mingange alisema atautumia mchezo huo ili kuwaandaa vijana wake wakafanye vema kwenye mchezo huo ambao utatoa mwakilishi wa msimu ujao kwenye kombe la shirikisho Afrika.

“Tunataka kumaliza msimu na kombe hilo ni jambo ambalo kila mmoja wetu lipo kichwani mwake, hatuna chetu kwenye Ligi hivyo uwepo wa mchezo dhidi ya Yanga utakuwa sehemu ya maandalizi.

“Kikosi kipo katika hali nzuri na kila mchezaji anaonekana kuwa kwenye morali ya juu, nachoomba ni wachezaji wangu kutopata majeraha yanayoweza kunivurugia hesabu zangu,” alisema Mingange.