Aussems nilikwenda kuzungumza na Tottenham Spurs

Muktasari:

Aussems aliyerejea Dar es Salaam jana usiku alikuwepo katika mazoezi ya asubuhi yaliyoanza saa 4:30 asubuhi huku mvua ikinyesha kwenye Uwanja wa Uhuru alisema aliondoka kwa matatizo binafsi hivyo anaweza kusema alikwenda kuzungumza na Spurs.

Dar es Salaam.Kocha wa Simba, Patrick Aussems amerudi na kusimamia mazoezi ya leo asubuhi huku akitania kwamba alikwenda kufanya mazungumzo na Tottenham Spurs iliyokuwa inatafuta kocha.

Kauli hiyo ya Aussems imekuja kutokana na kuulizwa alikwenda wapi kwa siku tatu bila ya kuaga uongozi wa klabu hiyo na kuzua taharuki juu ya hatma yake ndani ya klabu hiyo.

Aussems aliyerejea Dar es Salaam jana usiku alikuwepo katika mazoezi ya asubuhi yaliyoanza saa 4:30 asubuhi huku mvua ikinyesha kwenye Uwanja wa Uhuru alisema aliondoka kwa matatizo binafsi hivyo anaweza kusema alikwenda kuzungumza na Spurs.

"Siyo kila kitu anatakiwa kukiweka wazi kwa maana mambo mengine ni siri ya mtu binafsi kama ambayo ilikuwa kwangu kwahiyo kueleza nilipokwenda hilo nadhani si sahihi," alisema Aussem.

Nina uwezo wa kusema nilikwenda kuzungumza na Tottenham Spurs ya Uingereza ambayo ilikuwa inatafuta kocha wakati huo.

"Kwa hiyo kuhusu suala la kuwepo taarifa za kwenda timu nyingine au niliondoka hapa nilikwenda kusaini timu nyingine hilo nadhani si sahihi kwa wakati huu kwani ndio maana nimerudi kutimiza majukumu yangu katika kituo cha kazi," alisema Aussems.

Akizungumzia mazoezi hayo Aussems alisema aliacha mpango kazi wa kufanyika kwa ajili ya maandalizi ya mchezo wa ligi dhidi ya Ruvu Shooting.

"Hali ya timu kwa muda ambao nimeicha inakosa ufanisi mzuri katika kufanya mazoezi kutokana na mvua ambazo zinawapa changakoto katika viwanja vyao vya mazoezi ambavyo wanatumia," alisema.

"Liliopo mbele yangu wakati huu ni kupata ushindi dhidi ya Ruvu, ambao natambua ni timu nzuri kwani wamepata ushindi dhidi ya timu za KMC, Yanga na Azam ambao ziliwakilisha nchi katika mashindano ya kimataifa," alisema Aussems.