Asha Baraka aachia kiti Twanga Pepeta, Luiza Mbutu, Chaz Baba, Kalala Junior, Diouf wala mashavu

MMILIKI wa Kampuni ya African Stars Entertainment (ASET) amempasia kijiti cha ukurugenzi wa bendi ya Twanga Pepeta, Luiza Mbutu, katika mabadiliko makubwa ya kuiongozi ndani ya bendi hiyo.  

Muimbaji Luiza Mbutu amepandishwa cheo kutoka kuwa kiongozi wa bendi hadi Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bendi wakati Asha Baraka amekuwa mwenyekiti wa bendi hiyo.

Akizungumza na MCL Digital, Hassani Rehani amesema mabadiliko hayo yanamaanisha kwamba Asha Baraka hatafanya shughuli za kila siku za bendi na badala yake jukumu hilo limekabidhiwa kwa Luiza.

Rehani amesema mabadiliko mengine ya kiungozi ni kuwa Kalala Junior amekuwa Kiongozi Mkuu wa Bendi ambaye awali alikuwa Kiongozi Msaidizi wa Bendi.

Nafasi yake ya usaidizi imechukuliwa na Said Msafiri ‘Diouf’ ambaye alikuwa msimamizi wa jukwaani (Stage Master).

Nafasi ya ‘Stage Master’ ya Msafiri Diouf imechukuliwa na Charles Gabriel ‘Chaz Baba’ ambaye alikuwa hana cheo, huku Kiongozi wa Madansa anaendelea Super Nyamwela na msaidizi wake Maria Soloma.

 Mpiga gitaa Jumanne Jojoo ‘Jojoo Jumanne’ amekuwa mshauri wa bendi, huku Martin Sospeter na Hassan Rehani wanaendelea na nafasi ya umeneja wa bendi.

 Hata hivyo, Hassan Rehani amesema Asha Baraka amechukua hatua ya kujiondoa Ukurugenzi ili wanamuziki waweze kujiongoza wenyewe.