Dakika 45: Kipa Coastal Union aigomea Yanga Uwanja Mkwakwani ngoma suluhu

Muktasari:

Yanga imetawala mchezo katika kipindi cha kwanza pamoja na kupata kona tisa (9) na kushindwa kuzitumia huku wenyeji Coastal wakipata kona moja.

Tanga. Makipa Soud Abdallah wa Coastal Union na mwenzake Mechata Mnata wa Yanga wameonyesha kiwango cha juu na kuzifanya timu hizo kwenda mapumziko zikiwa suluhu kwenye Uwanja wa Mkwakwani.

Katika mchezo huo uliokuwa na upinzani kipa wa Coastal Union, Abdallah alifanya kazi nzuri kuokoa hatari za washambuliaji wa Yanga katika dakika zote walizokuwa wakishambuliwa.

Kipa Abdallah aliokoa mpira wa juu uliopigwa na Benard Morrison pia aliokoa mashambulizi ya washambulia Tariq Seif na Ditram Nchimbi.

Naye kipa Mechata wa Yanga alifanya kazi nzuri kumzuia Ayoub Lyanga asifunge bao baada ya Coastal Union kufanya shambulizi la kushtukiza.

Yanga watajilaumu wenyewe kwa kutawala mchezo katika kipindi cha kwanza pamoja na kupata kona tisa (9) na kushindwa kuzitumia huku wenyeji Coastal wakipata kona moja.

Katika mchezo mingine ya Ligi Kuu Tanzania Bara hadi sasa mapumziko; Tanzania Prison imeshinda 1-0 dhidi Lipuli kwenye Uwanja wa Jamhuri, Dodoma shukrani kwa bao Salum Kimenya.

Alliance FC ikiwa nyumbani imekwenda mapumziko ikiwa mbele kwa bao 1-0 dhidi ya Singida United kwenye Uwanja wa Nyamagana, Mwanza.