Real Madrid hesabu zao zote kwa Pochettino

Muktasari:

Kocha wa Real Madrid, Zidane hii ni awamu yake ya pili kwenye kikosi hicho, lakini mambo yametibuka na kutishia usalama wa kibarua chake baada ya kichapo cha mabao 3-0 ilichokipata timu yake kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya kutoka kwa Paris Saint-Germain.

LONDON, ENGLAND. Real Madrid wameripotiwa kwamba wanaendelea kumtazama kocha wa Tottenham Hotspur, Mauricio Pochettino kuwa ni chaguo lao la kwanza watakapomfuta kazi Zinedine Zidane.
Kocha wa Real Madrid, Zidane hii ni awamu yake ya pili kwenye kikosi hicho, lakini mambo yametibuka na kutishia usalama wa kibarua chake baada ya kichapo cha mabao 3-0 ilichokipata timu yake kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya kutoka kwa Paris Saint-Germain.
Taarifa mbalimbali zimekuwa zikielezwa kuhusiana na kipigo hicho na hali ya usalama wa kibarua cha Zidane huko Bernabeu, ambapo kocha wa zamani wa wababe hao wa Bernebau, Jose Mourinho, ambaye kwa sasa hana kazi aliripotiwa kwamba angerudishwa kuchukua mikoba.
Kwa mujibu wa The Mirror, Pochettino ndiye anayepewa nafasi kubwa ya kwenda kuchukua mikoba huko Bernabeu, wakiamini kwamba hata mshahara wake hautakuwa mkubwa sana, kwamba watamlipa Pauni 8.5 milioni kwa mwaka.
Spurs ya Pochettino ilikuwa kwenye ubora wake msimu uliopita ikifika fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya na kufungwa na Liverpool huko Madrid na mabosi wa Los Blancos wanaamini itakuwa vyema kama atakwenda kumbadili Zidane huko Bernabeu.