KMC kuichezesha AS Kigali saa 9 alasiri Uwanja wa Taifa

Muktasari:

KMC inahitaji ushindi wa aina yoyote ili kusonga mbele katika mashindano hayo

Dar es Salaam. Mechi ya mzunguko wa awali baina ya timu ya soka ya Manispaa ya Kinondoni (KMC) na AS Kigali ya Rwanda imepangwa kuanza saa 9.00 alasiri.

Mechi hiyo iliyopangwa kufanyika kwenye Uwanja wa Taifa, itakuwa ya marudiano ambapo katika mchezo wa awali, timu hizo zilitoka suluhu.

Afisa habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Clifford Ndimbo alisema muda huo umepangwa wa timu ya KMC na tayari Shirikisho la Soka Afrika (CAF) limeupitisha.

Tayari KMC imebadili ratiba yake ya mazoezi na sasa inafanya kuanzia saa 8.45 mchana kwenye uwanja wa Kijitonyama jijini.

Taarifa zimesema kuwa sababu ya mchezo huo kufanyika katika muda huo ni mikakati ya ushindi kwani hali ya hewa ya Kigali kwa sasa ni baridi.