Tambwe njia nyeupe kutimkia Uarabuni

Muktasari:

Mshambuliaji huyo ameachwa na Yanga msimu uliopita baada ya kuandamwa na majeruhi ya muda mrefu.

Dar es Salaam. Mshambuliaji Mrundi Amiss Tambwe yuko mbioni kujiunga na klabu ya Fanja FC ya Oman.

Tambwe aliyecheza kwa mafanikio katika klabu za Simba na Yanga na kuwa mfungaji bora wa Ligi Kuu Bara mara mbili katika msimu wa 2013/2014 na 2015/2016.

Anatimkia Fanja baada ya kumaliza mkataba wake na Yanga mwishoni mwa msimu uliopita 2018/2019.

"Kwa sasa tupo Burundi, tumeshaanza kuzoea mazingira, lakini Tambwe anatarajia kuondoka kwenda Oman kujiunga na Klabu ya Fanja muda wowote. Mipango ya safari kila kitu tayari,"alisema mke wake Tambwe anayeitwa Raiyan ‘Ray wa Tambwe’.

Raiyan ni Mtanzania mwenye asili ya Arabuni alikutana na Tambwe nchini alipokuja kucheza na kufunga ndoa miaka miwili iliyopita.

Kutua kwa Tambwe katika klabu ya Fanja ya Oman anakuwa si mchezaji wa kwanza kutoka kwenye Ligi Kuu Bara kucheza ligi hiyo.

Wachezaji wengine ni Mkongo Mbuyu Twite, Waivory Coast mapacha Kipre Tchetche ambaye kwa sasa ametimkia Malasyia na Kipre Bolou. Wengine ni wazawa Danny Lyanga na Yusuf Macho.