Kipa mkongwe Idd Pazi: Nimepata sifa kufundisha Ligi Kuu

Muktasari:

Pazi enzi zake alicheza kwa kiwango bora na baada ya kustaafu alifundisha timu mablimbali za soka nchini kutokana na uzoefu wake tu.

Dar es Salaam.Kipa wa zamani wa Simba na Taifa Stars, Idd Pazi amesema yuko huru kufundisha timu yoyote ya Ligi Kuu kama kocha wa makipa hivi sasa.

Pazi amebainisha hayo muda mfupi baada ya kuhitimu kozi ya ukocha ya intermediate ambayo iliendeshwa na mkufunzi, John Simkoko jijini Dar es Salaam.

"Nilikuwa nakosa sifa ya kufundisha kwenye timu za Ligi Kuu kama kocha wa makipa, kuna timu zilinikataa kutokana na vyeti japo uwezo nilikuwa nao.

"Nimejiongeza nikarudi darasani ambapo nilianza mwanzo kabisa kwani sikuwa na sifa yoyote ya ukocha, nimesoma na sasa nimehitimu kwa ngazi ya intermediate," alisema.

Kipa huyo wa zamani wa Stars amesema hivi sasa yuko huru kufundisha timu yoyote ile na kama wapo watakaomhitaji wamfuate.

"Wasihofu kuhusu vyeti vyangu, awali kila timu iliyonitaka TFF (Shirikisho la Soka Tanzania) ilinikata, waliniambia nikasome, mwanzo niliona tabu, lakini baadae nilikata shauri nikarudi darasani," amesema.