Kimbau: Mwakinyo aligomea pambano kisa dola 20,000

Muktasari:

Mwakinyo amepata umaarufu baada ya kumchapa Sam Eggington aliyekuwa bondia namba nane wa dunia kwenye uzani wa super welter, pambano lililoacha mshtuko nchini Uingereza Septemba mwaka Jana.

Dar es Salaam. Promota wa ngumi nchini, Shomari Kimbau amesema alimtafutia pambano bondia Hassan Mwakinyo ambalo lilikuwa na dau la dola 100,000 bondia huyo akaligomea sababu ya kutakiwa kumlipa Kimbau dola 20,000 kama Matchmaker.

Mwakinyo bondia namba moja wa Afrika kwenye uzani wa super welter na bondia wa 19 wa dunia aliweka dau la kucheza si chini ya dola 100,000, miezi michache baada ya kumchapa Samm Eggington wa Uingereza kwa TKO na kupanda kwenye ubora wa dunia.

Licha dau hilo la Mwakinyo, Promota wa ngumi nchini, Shomari Kimbau amesema aliwahi kumtafutia bondia huyo pambano la fedha hiyo ingawa Mwakinyo angechukua dola 80,000 na Kimbau dola 20,000 lakini akaligomea.

"Ilikuwa apigane na Jamie Munguia (bondia namba moja wa dunia kwenye uzani wa super welter), kila kitu kilikwenda vizuri na Mwakinyo nilizungumza naye nikamueleza na ofa waliyotoa ambayo mimi (Kimbau) nilipaswa kupata dola 20,000 kama matchmaker, lakini alikataa akataka apewe yote dola 100,000 pambano likaishia hapo," alisema.

Ingawa Mwakinyo amesisitiza kuwa hawezi kugomea ofa yoyote ambayo itafuata taratibu akisisitiza kwamba, yeye Mwakinyo ana menejimenti yake kwa anayetaka kumuandalia pambano inabidi apitie huko huku akisisitiza, dau lake haliwezi kuwa chini ya dola 100,000.