Azam yamnasa mshambuliaji wa Ivory Coast

Muktasari:

Ella anakuwa raia wa nne wa Ivory Coast kuichezea Azam FC akifuata nyayo za Kipre Tchetche, Kipre Balou na Paschal Wawa.

Dar es Salaam. Azam imefunga usajili wake kwa kishindo baada ya kumnasa mshambuliaji wa Ashanti Gold, Daly Ella Richard Djodi mwenye umri wa miaka 28.

Mshambuliaji huyo aliyewahi kuzichezea pia timu za Hire FC, Stella Club, SOA, Horoya na AC Leopards amejiunga na Azam kwa mkataba wa mwaka mmoja ambao una kipengele cha kuongezwa ikiwa klabu hiyo itaridhishwa na uwezo wake.

Ofisa Habari wa Azam, Jafar Iddi alisema kuwa usajili wa Djodi umefanywa kutokana na mapendekezo ya benchi la ufundi kwa ajili ya kuimarisha safu ya ushambuliaji.

"Wakati tunakwenda dakika za mwisho kwenye usajili, tumemuongeza mchezaji wa kimataifa kutoka Ivory Coast anaitwa Daly Ella Richard. Huyu ni straika. Kama mnavyofahamu kwamba tuna upungufu upande wa washambuliaji kwa hiyo ameongezwa mchezaji mwingine wa kimataifa.

Atakuwa ndio mchezaji wa mwisho kusajiliwa msimu huu. Ni mchezaji ambaye anatokea kwenye timu ya Ashanti Gold.

Ni kijana mdogo ambaye ana kasi nzuri na uwezo mkubwa. Amecheza klabu mbalimbali hadi anakuja Azam kwa hiyo ni matumaini yetu mwalimu atazidi kuimarisha kikosi chake upande wa ushambuliaji. Na sasa ni kwamba tunafunga rasmi zoezi la usajili kabla ya dirisha kufungwa," alisema Iddi.

Ni wazi kwamba Ella anakwenda kuchochea ushindani kwenye safu ya ushambuliaji ya Azam ambayo pia ina nyota kama Donald Ngoma, Obrey Chirwa, Iddi Seleman 'Nado', Emmanuel Mvuyekure na Seleman Ndikumana.