Mwinjuma Muumini anarudi upya na ‘Nimefulia’

Muktasari:

Katika sherehe ya miaka 30 atazindua albamu yake itakayobebwa na jina la wimbo wake huo mpya wa ‘Nimefulia’ itakuwa na nyimbo sita

Dar es Salaam.Baada ya kimya cha muda mrefu nyota wa muziki wa dansi nchini Mkurugenzi wa bendi ya Double M Plus, Muumini Mwinjuma ametangaza kurejea na wimbo ‘Nimefulia’, huku akiandaa sherehe ya kutimiza miaka 30 tangu aanze muziki.

Alisema katika sherehe hiyo ya miaka 30 atazindua albamu yake itakayobebwa na jina la wimbo wake huo mpya wa ‘Nimefulia’ na itakuwa na nyimbo sita ambazo tayari zishakamilika.

Muumini alisema anampango wa kutoa video katika wimbo huo kwani mashabiki zake wamekuwa wakimtaka aonekana kwanye video akiwa na muonekano wa sasa kwani ni muda mrefu hajaonekana na mara ya mwisho ilikuwa mwaka 2012 katika video ya wimbo wa ‘shamba la bibi’

“Hivi karibuni naachia wimbo wa Nimefulia huu utabeba albamu na nitafanya uzinduzi katika miaka 30 toka nimeanza muziki, na hata hivyo nitakavyoachia Audio sitakaa sana nitaachia na video sababu mashabiki zangu wengi wananiambia wamenimisi kuniona Katina video maana mara ya mwisho ilikuwa mwaka 2012 katika wimbo wa shamba la bibi,” alisema Muumini.

Aidha Muumini ambaye kwa nyakati  tofauti aliwahi kupitia bendi za Bantu Group, African Revolution 'WanaTamtam', Mchinga Sound 'Wana Kipepeo', Double M Sound, Mafahari Watatu,The African Stars 'Twanga Pepeta' na Victoria Sound ,amesema nyimbo zake za zamani kama Tunda, Maisha Kitendawili, Ndugu lawama, Mgumba, Kilio cha yatima, Mgumba part 2 na nyingine nyingi haziwezi kuchuja hata akitoa nyimbo mpya sababu kutokana na kuwa na hazina kubwa inamlinda ya nyimbo hizo kuendelea kufanya vizuri  na ndio maana mashabiki huziomba katika shoo yao.

“Unajua hata nikitoa nyimbo mpya kiasi gani bado mimi nina hazina kubwa inanilinda tunapiga nyimbo mpya sasahivi majukwaani zinazofanya vizuri, lakini bila kuwapigia watu tunda,mgumba maisha kitendawili na nyingine nyingi mashabiki wanakuwa hawakuelewi

“Leo watu sio watunzi wa nyimbo na wanaishi kwa nyimbo za kina hayati Mbaraka Mwishehe, Marijani Rajabu, na wanamuziki wengine wakongwe sembuse? mimi na nyimbo zangu mwenyewe zile nyimbo haziwezi kuchuja sababu zilifanya vizuri na sio ujumbe ule wa bigiji wa siku tatu umeisha ,na hicho ndicho kitu kinachonifanya naishi vizuri na najivunia kazi yangu niliyoifanya mimi bila kupiga nyimbo mpya jukwaani,” alisema Muumini.

Hata hivyo Muumin alisema “Pamoja na figisu figisu za hapa na pale katika muziki huu wa dansi ,unajuwa kuna watu hawataki kuisikia muziki wa dansi, ila  hawajui muziki huu ndio wenye visa vya ukweli na dansi ndio muziki baba na ndio muziki mama tofauti na muziki wa kubuni kukaa kwenye Kompyuta dakika mbili unatunga.”