Mo Salah awatosa kweupe Juventus, Real Madrid

Muktasari:

Salah amekuwa na kiwango cha juu tangu ametua Liverpool na ameweka wazi kuwa msimu ujao ndoto yake ni kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu England

London, England. Mshambuliaji wa kimataifa wa Misri, Mohamed Salah amekataa ofa ya kujiunga na Real Madrid na Juventus kwa kusema ataendelea kukipiga na majogoo wa jiji Liverpool.

Imeripotiwa kuwa nyota huyo anawindwa kwa Paundi 150 ili wamng’oe kwa mabingwa hao wa Ligi ya Mabingwa Ulaya majira haya ya kiangazi barani Ulaya.

Miamba hiyo ya soka la Hispania na Italia, wameandaa kiwango kikubwa cha fedha, wanatakiwa kusubiri hadi pale utakapomalizika msimu ujao wa 2019/20.

Kocha wa Liverpool, Jurgen Klopp anatajwa kuwa baada ya msimu kumalizika walikaa chini na vigogo wa klabu hiyo kwaajili ya kuweka mikakati ya kuwazuia nyota wao.

Inadaiwa kuwa Salah ambaye yupo na timu yake ya taifa ya Misri kwaajili ya kujiandaa na fainali za AFCON aliongea na vigogo wa Liverpool ambao aliwaeleza kuwa huu sio muda sahihi kwake kuondoka.

Salah na pacha wake Sadio Mane baada ya kuiongoza Liverpool chini ya  Jurgen Klopp kutwaa ubingwa wa Ligi ya Mabingwa sasa watakuwa na vibarua vya kupigania mataifa yao mwezi huu katika AFCON.