Aiyee ageuka lulu, simu za mabosi zamiminika

Muktasari:

Mshambuliaji huyo amekuwa na msimu mzuri katika kikosi cha Mwadui kwa kufunga jumla ya mabao 18 katika ligi pamoja na mechi za mtoano

Mwadui.Baada ya kumaliza Ligi Kuu akiwa na mabao 16, na kuinusuru timu yake ya Mwadui FC kushuka daraja mshambuliaji Salim Aiyee ameanza kupokea simu kutoka vigogo wa klabu mbalimbali wakitaka huduma yake.

Aiyee ameibeba Mwadui FC hasa baada ya kufunga mabao mawili katika mchezo wa mtoano wa kuwania kubaki Ligi Kuu dhidi ya Geita Gold.

Mwadui FC ililazimika kucheza ligi ya mchujo baada ya kumaliza ligi kuu ikiwa na pointi 44 sawa na Kagera Sugar ambao wamebaki msimu ujao kwa kuifunga Pamba FC ya jijini Mwanza.

Aiyee alisema baada kufumania nyavu msimu huu kwa kasi kubwa timu nyingi kutoka ndani na nje ya Tanzania zimeanza kumtolea macho ambapo ameweka wazi kuwa ana lengo la kuondoka Mwadui.

"Mkataba wangu na Mwadui umeisha, mpaka sasa nimepokea ofa nyingi zingine zinatoka nje ya nchi, bado sijafanya uamuzi nitaenda wapi au nitabaki hapahapa, sehemu nitakayokubaliana nayo ndio nitajiunga nayo " alisema Aiyee.

Mshambuliaji huyo alisisitiza kuwa mpira wa miguu ni kazi hivyo yeye kama mfanyakazi atakuwa tayari kutumikia sehemu ambayo itakuwa na maslahi zaidi.

“Hii ndio kazi yangu niliyoichagua hivyo lazima niiheshimu nitaangalia mahala ambapo kutakuwa na maslahi makubwa kwangu na sio kingine,” alisema Aiyee.