Zidane akatisha utawala wa Bale ndani Real Madrid

Muktasari:

Bale amekuwa katika wakati mgumu katika kikosi cha Real Madrid kutokana na kusumbuliwa na majeraha ya muda mrefu

London, England. Mwaka mmoja uliopita, Gareth Bale alifunga bao tamu katika mchezo wa fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, lakini sasa hana thamani tena kwa Kocha Zinedine Zidane.

Bale hana furaha kama aliyokuwa mwaka mmoja uliopita katika kikosi cha Real Madrid tangu alipoibua mzozo na Zidane.

Tangu Mei mwaka jana, Bale na Zidane hawazungumzi na kila mmoja anaangalia maisha yake ndani ya klabu hiyo tajiri Hispania.

Zidane baada ya kurejea Real Madrid kwa mara ya pili alimtaka Bale kusaka timu mpya majira ya kiangazi, vinginevyo atamtoa kwa mkopo.

Hata hivyo, hakuna klabu ya Ulaya iliyoonyesha dhamira ya kutaka huduma ya nyota huyo wa zamani wa Tottenham Hotspurs.

Katika kuthibitisha wawili hao hawaivi chungu kimoja, Zidane alimuweka benchi Bale katika mchezo wa mwisho wa kumaliza msimu waliochapwa mabao 2-0 na Real Betis nyumbani kwenye Uwanja wa Santiago Bernabeu.

Mchezaji huyo wa kimataifa wa Wales, alishindwa kuaga mashabiki wa klabu hiyo na alinekana mnyonge alipokuwa akiingia ndani ya vyumba vya kuvalia nguo baada ya mechi kumalizika.