Mapicha picha ya mama yamtibua mwanasoka

Muktasari:

Mama huyo, Francesca Costa mwenye umri wa miaka 41 ana zaidi ya wafuasi 169,000 kwenye ukurasa wake huo wa mtandao ya kijamii

ROME, ITALIA. Chipukizi wa AS Roma, Nicolo Zaniolo amelazimika kutumia muda wake kumkumbusha mama yake mzazi kwamba umri umeshakwenda hivyo aache kupiga selfie za kichokozi na kisha kuzituma kwenye ukurasa wake wa Instagram zinakwaza.
Mama huyo, Francesca Costa mwenye umri wa miaka 41 ana zaidi ya wafuasi 169,000 kwenye ukurasa wake huo wa mtandao ya kijamii, lakini picha zake anazoposti zinamfanya mtoto wake kukosa raha.
Zaniolo amekuwa kwenye kiwango bora kabisa kwa sasa akitamba katika kikosi cha AS Roma baada ya kunaswa kutoka Inter Milan kwenye dirisha la majira ya kiangazi la mwaka jana. Mchezaji huyo, ambaye amepachikwa jina la Totti mpya, alifunga mabao yote yaliyofungwa na AS Roma kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya FC Porto wiki iliyopita. Msimu huu amecheza mechi 22 katika michuano yote akiwa na kikosi hicho cha AS Roma na kufunga mabao matano jambo lililompa nafasi ya kuitwa kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Italia, Azzurri.
Lakini, kwa sasa akianza kutambulika zaidi, amemwomba mama yake, ajaribu kubadiliko huko kwenye mitandao ya kijamii na kuacha kuposti picha za kutamanisha. Hivi karibuni mama huyo alipiga selfie akionyesha busu jambo lililomkera mwanaye.
"Unafanya nini na mdomo wako kama hivyo? Wewe una miaka 40!" yalikuwa maneno ya mtoto Nicolo akimwambia mama yake.
AS Roma sasa inafanya kila wanaloliweza kumfanya kinda wao huyo matata kabisa kutofuatilia kabisa mambo ya kwenda mitandao ili asiharibu kiwango chake bora kabisa kinachomfanya awe na mashabiki wengi huko Stadio Olimpico.