Mtibwa Sugar washindwe wao tu

Muktasari:

Mtibwa wameingia katika hatua ya pili ya kombe la Shirikisho Afrika baada yaa kuwatoa klabu ya Northern Dynamo kwa jumla ya mabao 5-1.

Dar es Salaam. Mtibwa Sugar imefanikiwa kusonga mbele katika mashindano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika, baaada ya kuichapa Northern Dynamo kwa jumla ya mabao 5-1.

Katika raundi ya pili Mtibwa wanakuwa na kibarua kingine dhidi ya KCCA inayoshiriki Ligi Kuu nchini Uganda, huku klabu hiyo ikionekana kuwa imepania kufanya vizuri katika mashindano haya.

Mwanaspoti limeangalia baadhi ya vitu ambavyo Mtibwa wanatakiwa kufanya ili kuhakikisha kwamba wanaweza kusogea mbele zaidi na kushangaza watu.

KAMBI YA MAANA

Mabosi wa Mtibwa wanatakiwa kuhakikisha wanawapeleka katika kambi nzuri ambayo itaawafanya wachezaji wake wakae na kutuliza akili zao.

Wanatakiwa kuhakikisha kwamba wanawaweka wachezaji wao katika mazingira mazuri kuanzia sehemu ya kulala na uwanja salama ambao wanaweza wakafanya mazoezi kwa muda sahihi.

Kukaa kwao kwenye mazingira hayo kutawafanya wachezaji kisaikolojia wawe vizuri kwasababu kutakuwa hakuna buguza yoyote inayowakabili pindi watakapokuwa kambini.

Hata hivyo imetajwa kwamba Uongozi wa klabu hiyo umefikilia kuwapeleka wachezaji wake katika kambi ya Sobibo (Kagera), ambayo inatumiwa na klabu ya Kagera Sugar.

MOTISHA

Hiki ni kitu ambacho timu nyingi hutumia pindi ambapo wanahitaaji maatokeo katika mchezo husika. Mtibwa wanabidi wapambane kuhakikisha wachezaji wao wanapata posho.

Timu hii ilichukua ubingwa wa kombe Fa msimu uliopita lakini zawadi zao imekuwa danadana, hivyo wanachotakiwa kuhakikishaa mabosi wa Mtibwa ni kuwa tofauti kwa kuwapa motisha (Posho) ambazo zitawabusti katika kipindi hiki.

Wana kampuni naa wadau wengi ambao wanaweza kuisaidia pesa timu hiyo katika kipindi hiki kwasababu wameanza vizuri Mashindano hivyo wanaweza kutumia kama njia ya kujitangaza kupitia jezi zao.

UMOJA

Kitu kingine ambacho kinahitajika sehemu yoyote ni umoja na ushikamano. Kama kuna migogoro ya chini kwa chini inayoendelea hivi sasa ndani ya mtibwa ni bora wakaachana nayo.

Kipindi hiki ni sawa na kipindi cha mavuno kwa sababu wote wanatakiwa kuvuna ili kupata mazao, wachezaji wa Mtibwa wanahitajika kupambana vilivyo ili kusogea mbele.

Umoja ndio utawafanya wasogee mbele, lakini kama wakianza kutengeneza matabaka katika kipindi hiki basi ni ngumu mno kwa wao kusogea mbele kutokana na kila mmoja atataka kuonyesha uwezo wake pekee.