#UCHAGUZI SIMBA: Kaduguda arejea ukumbini

Muktasari:

Kaduguda amewahi kuwa katibu mkuu wa Simba kipindi Cha utawala wa mwenyekiti Hassan Dalali.Pia ni Mwalimu wa shule ya Sekondari Jitegemee.

Dar es Salaam. Wanachama wachache wamemsihi mgombea ujumbe katika klabu ya Simba, Mwina Kaduguda arejee ndani ya Ukumbi kuendelea na Uchaguzi.

Kaduguda alizua sekeseke ukumbini kwa dakika kadhaa baada ya kupinga idadi ya wanachama wanaotakiwa kupinga kura.

Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya Simba, Boniface Lyamwike awali alitangaza idadi ya wapiga kura ni 1720 na badaye akabadilisha akasema 1728.

Baada ya kutangaza hivyo ndipo Kaduguda akasimama kwenda meza kuu akipinga idadi hiyo ya wapiga kura na kusema idadi ni 1486 iliyotajwa awali na hajui hao wengine wametoka wapi.

Kutokana na hilo ilibidi Kaduguda atolewe nje na Polisi na alisikika akisema yeye hajafanya kosa lolote kuuliza kwani ni haki yake lakini anashangaa Polisi wanakuja kumtoa.

Alipofika nje wakati akielekea kutoka kabisa nje ya eneo hilo baadhi ya wanachama walimsihi kwa muda mrefu apunguze hasira na arejee ndani kuendelea na mchakato wa Uchaguzi.

Kaduguda aliwasikiliza na kurejea ukumbini akisindikizwa na baadhi ya wanachama na Polisi mmoja na moja kwa moja akaenda meza kuu na kukumbatiana na Kaimu Rais wa Simba, Salim Abdallah 'Try Again' na kuamsha shangwe kutoka kwa wanachama.