Nonga: Mabeki wanakaba mpaka kivuli changu

Muktasari:

Nonga hadi sasa ameingia kambani mara saba akiwa nyuma kwa bao moja tu dhidi ya kinara wa upachikaji wa mabao Meddie Kagere ambaye ameingia kambani mara 8.

NAHODHA wa Lipuli FC, Paul Nonga ametaja sababu za kushindwa kuingia kambani kwenye michezo miwili mfululizo kuwa ni kukamiwa na mabeki wa timu pinzani.

Nonga ambaye ndiye kinara wa upachikaji mabao ndani ya Lipuli hajafunga mechi dhidi ya Kagera Sugar na Biashara United.

Nonga alisema mabeki wamemjua kama ndiye mwenye madhara kwenye timu hivyo wamekuwa wakimkaba na kumnyima nafasi ya kuisaidia timu kuipa matokeo mazuri.

"Kukabwa kwangu kunanipa changamoto ya kupambana zaidi hakunikatishi tamaa ndio kwanza wananiongezea morali ya kutafuta mbinu kuhakikisha nafikia malengo kama nilivyokusudia kuhakikisha nakuwa na wastani mzuri wa kufunga,"

"Nadhani mwalimu pia ameliona hilo la mimi kudhibitiwa hivyo kuna umuhimu wa kuongeza nguvu zaidi kwenye safu yetu ya ushambuliaji ili nikibanwa mwingine apate upenyo wa kufunga hili linaweza kuwa muhimu zaidi timu kufikia malengo," alisema.