Kipchoge avunja rekodi ya dunia, Berlin Marathon!

Muktasari:

  • Hadi anakamilisha mzunguko wa kilomita 30, zikiwa zimesalia kilomita 12, tayari ilikuwa wazi ulimwengu unakwenda kushuhudia rekodi mpya ya dunia, kwani alikuwa amesalia na sekunde 52 tu kufanya maajabu.

Nairobi. Hatimaye mwanariadha, Eliud Kipchoge wa Kenya, amevunja rekodi ya Dunia, akitumia muda wa saa 2:01:40 na kushinda mbio za Berlin Marathon, zilizomalizika leo Jumapili muda mfupi uliopita nchini Ujerumani.

Kipchoge mwenye umri wa miaka 33, alihakikisha anaingia katika vitabu vya kumbukumbu na kuwa mwanariadha wa kwanza kumaliza mbio hizo akitumia muda wa chini ya saa 2:02:00.

Mwanariadha huyo, alipovuka utepe ndani ya sekunde 77 kabla ya muda huo 2:02:00 uliozoeleka.

Mkenya mwingine, Amos Kipruto, ambaye alikuwa anapigiwa upatu kutesa katika mbio hizo, alimaliza katika nafasi ya pili, akivuka utepe katika muda wa saa 2:06:22, huku mwenzao ambaye ni mshikilizi wa rekodi ya zamani, Wilson Kipsang akimaliza wa tatu akitumia muda wasaa 2:06:47.

Kipchoge ambaye alikuwa ametanguliwa na wanariadha wengine, aliwashanga wengi pale alipoamua kufyatuka na kuchupa hadi mbele, akitumia muda wa dakika 2:43, kukimbia umbali wa kilomita moja ya mwanzo.

Licha ya umri wake kuwa mkubwa, Kipchoge aliwaacha wenzake kwa mbali, akiandikisha muda bora kabisa wa dakika 14: 24, kumaliza mzunguko wa kilomita tano, kabla ya kuvuka kilomita 10, ndani ya

dakika 29:01.