Jinsi Madrid ilivyomnasa Hazard baada miaka 10

Muktasari:

Zidane alimtambua pia Raphael Varane, ambaye Real Madrid walimsajili mwaka 2011.

MADRID, HISPANIA.SUPASTAA, Eden Hazard yupo kwenye hatua za mwisho kabisa kukamilisha dili lake la kujiunga na Real Madrid miaka 10 tangu Zinedine Zidane alipowaambia wababe hao wa Bernabeu wamsajili Mbelgiji huyo.
Madrid wameripotiwa kukubali kuilipa Chelsea Pauni 130 milioni kupata huduma ya mchezaji huyo ambaye pia ni ndoto zake kwenda kuichezea timu hiyo kwenye La Liga. Na kwamba Hazard atakwenda kulipwa mshahara wa Pauni 400,000 kwa wiki.
Lakini, Los Blancos wasingekuwa kwenye madhara ya kutumia pesa nyingi hivyo kupata huduma ya Hazard kwa sasa kama wangemsikiliza Zidane wakati huo, kipindi winga huyo alipokuwa Lille.
Kipindi hicho Barcelona, Arsenal na Manchester United zilikuwa zikimtaka kabla ya kunaswa na Chelsea. Zidane hapo alikuwa ndio kwanza amestaafu soka na alikuwa akifanyakazi Real Madrid, japo haikuwa rasmi na alimwona Hazard, akatambua kipaji chake na akawaambia mabosi hao wa Bernabeu wakamsajili.

Zidane alimtambua pia Raphael Varane, ambaye Real Madrid walimsajili mwaka 2011.
Alimwambia Florentino Prez akamsajili Hazard, wakati huo akiwa na umri wa miaka 19 kwamba atakuja kuwa staa mkubwa baadaye, lakini bosi huyo akampuuza na kunasa wachezaji waliokuwa mastaa tayari kama Cristiano Ronaldo kutoka Man United na Karim Benzema kutoka Lyon.
Zidane, ambaye ni kocha wa Real Madrid kwa sasa, alisema: “Ningekuwa na uwezo kipindi kile ningemchukua Hazard nikiwa nimefumba macho."
Hazard alikwenda zake Chelsea, ambako alikutana na kocha Jose Mourinho na Madrid wao waliamua kumchukua Luka Modric. Lakini, sasa Zidane anaelekea kumpata mchezaji wake aliyetaka akachezee Los Blancos.